Mshambuliaji
 wa zamani wa Simba na timu ya taifa, Taifa Stars, Joseph Kaniki 
amepandishwa kizimbani jijini Addis Ababa, Ethiopia kutokana na tuhuma 
za kukamatwa na madawa ya kulevya.
Iwapo
 Kaniki pamoja na mwenzake Mkwanda Matumla ambaye ni bondia watapatikana
 na hatia, basi watafungwa nchini Ethiopia hadi watakapomaliza kifungo 
chao, Serikali ya Tanzania imethibitisha hilo.
Kaimu
 Balozi wa Tanzania nchini Ethiopia, Samuel Shelukindo ameliambia 
Championi Ijumaa, jana kutoka Addis Ababa kuwa, Kaniki na Mkwanda 
walipandishwa kizimbani kwa mara ya kwanza  mwanzoni mwa wiki na huenda ikawa hivyo tena wiki ijayo.
“Jana
 (juzi) tulikwenda kuwaona na tumekuwa tukifuatilia kwa karibu, huku 
kidogo kuna utaratibu tofauti, hivyo hatujajua lini watapandishwa tena 
kizimbani kwa mara ya pili.
“Iwapo
 watapatikana na hatia, kama ni kifungo cha jela, basi watatumikia hapa 
Ethiopia. Maana tunabanwa kutokana na kutokuwa na mkataba wa kupeana 
washitakiwa au wafungwa kama ambavyo nilieleza awali,” alisema 
Shelukindo.
“Hii
 juzi tu, kuna Watanzania wengine walikuwa wamefungwa hapa na tayari 
wameshamaliza vifungo vyao, wameondoka kurejea nyumbani.
“Lakini
 tumekuwa tukifuatilia kwa karibu, lengo ni kuhakikisha hata kama 
watuhumiwa au wakihukumiwa, basi haki yao inapatikana. Uingereza, 
Marekani na nchi nyingine wamekuwa wakifanya hivyo.”
Lakini
 taarifa nyingine ambazo gazeti hili limezipata kutoka kwa Mtanzania 
anayeishi Addis Ababa, zinaeleza Kaniki amekuwa akilia gerezani usiku 
kucha.
“Kuna
 Watanzania wenzetu wamefungwa katika gereza ambalo Kaniki yumo, 
tulienda kuwaona juzi, yeye hatukumuona. Ila wanasema amekuwa akilia 
usiku kucha, tena wakati mwingine kwa sauti ya juu akionekana kulijutia 
suala hilo,” alisema Mtanzania huyo ambaye hakupenda kutajwa jina lake 
gazetini.
Kaniki
 na Mkwanda walikamatwa siku kadhaa zilizopita kwenye Uwanja wa Ndege wa
 Kimataifa wa Bole, Addis Ababa nchini humo wakiwa njiani kwenda barani 
Ulaya na taarifa zinaeleza wangetua Italia, nyingine Hispania lakini 
wawili hao wanaishi Sweden.
Kaniki
 amewahi kuzichezea Simba, Mtibwa Sugar na Rayon Sports ya Rwanda, 
alikwenda kufanya majaribio Sweden ambako alifeli lakini baadaye 
akasajiliwa na timu ya daraja la pili ya Konya ambayo hata hivyo, 
hakudumu nayo na kazi yake ya mwisho ilikuwa ni ufagizi katika kampuni 
ya usajili mjini Norrkoping.
CHANZO: GAZETI LA CHAMPIONI
 

 
No comments:
Post a Comment