SAKATA la mawaziri kuandamwa kwa kutowajibika limezidi kushika kasi ambapo safari hii, Rais Jakaya Kikwete ametakiwa kumfukuza kazi Waziri Mkuu, Mizengo Pinda kwa madai ya kuwa mchawi wa maendeleo ya nchi na mzigo namba moja.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za 
Mitaa, Hawa Ghasia naye anadaiwa kuwa mzigo mwingine kwa taifa kutokana 
na kubariki ufisadi katika wizara yake.
Kauli hiyo ilitolewa jana na Mbunge wa Mwibara, Kangi Lugola (CCM) 
alipokuwa akichangia katika hoja mbalimbali kuhusu kamati tatu za Bunge 
zilizowasilishwa bungeni juzi.
Kamati zilizowasilisha hoja zao ni ile ya Hesabu za Serikali za Mitaa, Kamati ya Bajeti na Kamati ya Hesabu za Serikali.
Lugola alisema kama Rais Kikwete asipowafukuza kazi Pinda na Ghasia, 
CCM itakuwa shakani kurejea madarakani katika uchaguzi mkuu mwaka 2015.
“Mimi nawashangaa wabunge wenzangu mnaosimama hapa na kutumia nguvu 
zenu nyingi kuishauri serikali… hii serikali inayoongozwa na chama 
changu haishauriki, kwa kipindi kirefu ina watu wasiojua majukumu yao.
“Ni ngumu kuishauri serikali kutokana na kuwa na mawaziri wasiojua 
majukumu yao, kwa kutojua wanachokifanya wameamua kutohudhuria vikao 
muhimu vya kujadili taarifa za kamati,” alisema.
Lugola alisema katika kikao cha jana, mawaziri sita na manaibu wawili
 ndio waliohudhuria, hivyo waliobaki kukosa fursa ya kusikiliza michango
 mbalimbali inayotolewa na wabunge.
“Mimi ni mbunge wa CCM, na pengine haya ninayotaka kuyasema yanaweza 
yasiwapendeze wabunge wenzangu wa CCM, lakini ndivyo nilivyo, ndivyo 
Mungu alivyoniumba, naomba wanisamehe. Nchi nyingine katika Bunge 
Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) anapowasilisha 
taarifa, ndiyo wakati nchi nzima masikio ya watu yanakuwa bungeni, 
lakini kwetu ni tofauti,” alisema.
Wakati Lugola akichangia bungeni, walikuwepo mawaziri wanne tu na manaibu wawili, huku nafasi za mawaziri zikiwa wazi.
Waliokuwepo bungeni ni Waziri wa Maji, Profesa Jumanne Maghembe, Hawa
 Ghasia, Sofia Simba, Shamsi Vuai Nahodha, Mhandisi Charles Kitwanga na 
Janet Mbene.
“Lakini cha kushangaza kuanzia jana Waziri Mkuu ameenda kuhudhuria 
mahafali wakati jambo muhimu kama hili linazungumzwa bungeni. Hata hivyo
 pamoja na kuwa mheshimiwa spika jana (Juzi ) uliwatetea mawaziri kuwa 
walikuomba ruhusa, lakini mimi hainiingii akilini kuwa waliomba ruhusa 
mawaziri wote na kubaki mawaziri wanne na manaibu wawili,” alisema 
Lugola.
Alibainisha kuwa kwa busara za kawaida spika asingekubali kuwaruhusu 
mawaziri hao wakati kuna jambo la muhimu  linajadiliwa kwa mustakabali 
wa taifa na watu wake.
Lugola alisema TAMISEMI ina mtandao mkubwa wa utumiaji wa fedha ambao
 hauwezi kuwatenganisha Waziri Mkuu na Waziri Ghasia ambapo asilimia 70 
ya fedha za bajeti hupelekwa huko.
Alisema kuwa licha ya wizara hiyo kutengewa fedha nyingi, bado 
serikali imekuwa ikisuasua kushughulikia masuala mbalimbali ya wananchi 
wa kipato cha chini.
Lugola aliwataka wabunge wasiendelee kuwasaliti Watanzania kwa 
kubariki ufisadi unaofanywa na viongozi wa TAMISEMI inayoongozwa na 
Waziri Mkuu, Pinda.
Alibainisha kuwa kwa sasa serikali haishauriki, na jambo hilo 
linaonekana wazi kwakuwa imeendelea kulipa mishahara hewa kwa 
waliofariki, huku Watanzania wakiteseka kwa umaskini.
Lugola aliongeza kuwa serikali imekuwa ikibariki ununuzi usiokuwa na nyaraka jambo ambalo ni wizi, lakini unalindwa na viongozi.
“Mchawi wetu katika maendeleo serikalini, tatizo kubwa ni Waziri Mkuu
 amekuwa mpole mno, hawajibiki…, matatizo yanatokea ndani ya nchi yupo 
wapi? Wananchi Mwibara umaskini unakithiri, fedha zinaliwa ambazo 
zingewapa madawati, watu wangepata madawati na maji, wangevua kwa uvuvi 
wa kisasa, Waziri Mkuu, jamani nakulilia huko wapi uwajibikaji wako 
ndani ya serikali?” alisema.
Naye Mbunge wa Musoma Mjini, Vicent Nyerere (CHADEMA), alisema 
serikali imeshindwa kufanya kazi, hivyo ni vema Watanzania wakafanya 
uamuzi wa kuiondoa madarakani kwa kutumia sanduku la kura.
Alisema kinachoonekana kwa Serikali ya CCM ni kubariki ufisadi 
kutokana na viongozi waliopo madarakani kushindwa kuwawajibisha 
wanaobainika kufanya ufisadi kwa sababu ya kulindana.
Nyerere alisema aliyekuwa Waziri Mkuu, Edward Moringe Sokoine, 
alikuwa na uwezo wa kuwawajibisha waliobainika kufanya ubadhirifu wa 
mali za umma.
“Hapa serikali mnaweza kujipima kuwa hata nyinyi wenyewe 
mmeishajikatia tamaa kutokana na kukosa huduma za kiafya na ndiyo maana 
hata alipotokea babu wa Loliondo viongozi wote mlikimbilia huko kwenda 
kupata kikombe,” alisema Nyerere.
Katika mjadala huo ambao umeibua hisia kali kwa wabunge, ambao kwa 
asilimia kubwa wamekuwa wakilalama kuwa TAMISEMI kuna ufisadi mkubwa 
ambao unafanyika huku serikali ikiwa imenyamaza kimya.
Katika mjadala huo wabunge walikuwa wakihoji sababu za watendaji 
wanaotuhumiwa kufanya ubadhirifu kuhamishwa vituo vyao vya kazi badala 
ya kufikishwa kwenye vyombo vya sheria.
Mara kwa mara wabunge na viongozi wa CCM wamekuwa wakiwalalamikia 
mawaziri kwa kushindwa kuwajibika, hivyo kuisababisha serikali kuchukiwa
 na wananchi.
Wiki mbili zilizopita Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye
 alikaririwa akiwataja mawaziri wanne ambao wanatakiwa kutoa majibu ya 
uwajibikaji wao kwenye Kikao cha Kamati Kuu (CC) ya chama hicho 
kinachotarajia kufanyika wakati wowote kuanzia sasa.
Nape aliwataja mawaziri hao kuwa ni Waziri wa Kilimo Chakula na 
Ushirika, Christopher Chiza, naibu wake Adam Malima, Waziri wa Uvuvi na 
Mifugo, David Mathayo na Waziri wa Maji, Jumanne Maghembe.
 

 
No comments:
Post a Comment