Waona giza nene mbele yao, Uganda yaonya vita inanukia
DRC yazidisha mashaka kwa Uganda, Watanzania waonya
Hatua
 ya Serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC) kukataa kusaini 
mkataba wa amani na kundi la waasi la M23, imepeleka kilio kwa kundi 
hilo, na sasa wanalia njaa uhamishoni nchini Uganda.
Uganda, nchi ambayo ni msuluhishi wa mgogoro huo, imejikuta katika 
wakati mgumu kwani kundi la waasi wa M23 wapatao 1,700 limekimbilia 
nchini humo, ilhali Uganda ikiwa na jukumu la kusuluhisha waasi hao na 
Serikali ya DRC.
Msemaji
 wa Serikali ya DRC, Lambert Mende, mwishoni mwa wiki ametamka kuwa 
Serikali yake ina wasiwasi kuwa Uganda ina maslahi binafsi na waasi wa 
M23, hivyo hawako tayari kutia saini mkataba unaosimamiwa kwa mitego.
“Uganda sasa inaonekana kuwa sehemu ya mgogoro. Ina maslahi na M23,” alisema Mende. 
Kauli
 hii ya Mende imekuja siku chache baada ya DRC kukataa kutiliana saini 
na waasi kwa maelezo kuwa M23 ni kundi lililotangaza kujivunja, 
wamekimbilia Rwanda na Uganda, na hivyo kulipa sharti kubwa 
wanalolikataa.
Sharti
 hilo ni kuwa mkataba uwe na kipengele kinachowazuia M23 milele 
kutoshika silaha na kuanzisha mapambano, hoja inayokataliwa na waasi, 
huku Uganda ikizishawishi pande mbili zitie saini mkataba hivyo hivyo 
ulivyo kwa maelezo kuwa yakitokea matatizo mbele ya safari utarekebishwa
 tena.
Masharti
 mengine wanayowapa waasi hao ni kuwa makamanda wapatao 100 waliokuwa 
wanaongoza kundi la M23, wasiruhusiwe kuingia jeshini moja kwa moja, na 
badala yake wapewe mafunzo ya kijeshi, huku wakiacha fursa ya kushitaki 
wahalifu wa kivita watakaothibitika mbele ya safari kuwa walitenda 
uhalifu dhidi ya binadamu.
Uganda,
 ambayo sasa hivi ina mzigo mkubwa wa kulisha waasi hao waliowekwa 
kambini nchini humo tangu Jumatatu (Novemba 4) kundi hilo lilipotangaza 
kushindwa vita na kuweka silaha chini, inasema hali inayoiona ikiwa 
waasi hao hawatahakikishiwa usalama wao, pato la fedha na kushirikishwa 
serikalini, kuna wasiwasi kuwa wanaweza kurejea msituni.
“Hawa
 ni binadamu. Njaa ikiwashika, usitarajie watasubiri kufa kwa njaa. 
Wanaweza kurejea msituni,” alisema afisa mmoja wa Serikali ya Uganda.
Uganda
 pia imetishia kwa mara nyingine mwishoni mwa wiki kuwa ikiwa suluhu 
haitapatikana haraka, na DRC ikaendelea kuituhumu kuwa inashirikiana na 
waasi wa M23, basi yenyewe itajitoa katika nafasi ya kuwa msuluhishi.
Kuhusiana
 na tishio la Uganda kujitoa kwenye mazungumzo, Waziri Mdogo wa Mambo ya
 Nje wa Uganda, Asumani Kiyingi, amesema: “Tumewasiliana na Umoja wa 
Mataifa kupitia kwa Balozi wetu jijini New York, kwani tunataka kufahamu
 iwapo kilichoandikwa kwenye vyombo vya habari ni cha kweli,” amesema.
“Ikiwa
 Umoja wa Mataifa utathibitisha kuwa wataalamu wake wameandika taarifa 
hizo za uongo [kuwa Uganda inaunga mkono M23], basi tutajitoa katika 
jukumu la usuluhishi wa mgogoro wa DRC na waasi wa M23.”
M23
 kwa upande wao walioanza vita Aprili 2012 wanamtuhumu Rais Joseph 
Kabila kuwa wao ndiyo waliomsaidia baba yake, Laurent Kabila, kuingia 
madarakani na hata makundi ya waasi yalipokuwa yanatishia kumuondoa 
madarakani walimtetea, lakini alipoingia madarakani akawatekeleza.
Wataalamu
 wanasema kuwa nchi za Uganda na Rwanda pamoja na kukaripiwa na jumuiya 
ya kimataifa, zikaacha kukiunga mkono kikundi cha M23, hali iliyokifanya
 kichapwe kama mtoto mdogo, sasa zimehamishia nguvu kwa makundi mengine 
ya waasi yaliyopo kwenye misitu ya Congo.
Shutuma
 kubwa zinazosukumwa kwa nchi hizi ni kuwa zimekuwa zikinunua madini na 
mbao kutoka kwa waasi, hali inayoziingizia fedha nyingi za kigeni bila 
kujali kuwa zinahatarisha maisha ya Wakongo wasio na hatima, taarifa 
ambazo Serikali ya Uganda imeziita za ‘kipuuzi’.
Kikosi
 Maalum cha Umoja wa Mataifa kinachoongozwa na Mtanzania, Brigedia 
Jenerali James Mwakibolwa, kwa kuhusisha Brigedi Maalum ya SADC, 
kimewachakaza M23 hadi wakasalimu amri, lakini wachambuzi wa mambo 
wanasema kung’olewa kwa M23 si mwisho wa matatizo DRC.
Richard
 Mugamba, Mhariri Mtendaji wa gazeti la the Citizen, ambaye amekuwa 
akiripoti habari za waasi kwa kufika Goma, anasema M23 ni moja ya 
makundi zaidi ya 17 yaliyoko mashariki mwa Congo.
“Kila
 mtu anatambua kwamba M23 kuweka silaha chini ni furaha kwa Wakongo, ila
 matatizo yao yana miaka 17. Tangu 1999 wamekufa watu milioni 5. M23 
wamekuwapo kwa miezi 24, lakini mashariki mwa Congo kuna makundi kama 
FDRL, Mai Mai, RCD-Goma, ADF, kuna vikundi 17 na vyote hivi viko 
mashariki kwenye madini, kwenye mbao na mkaa.
“Ni
 vyema kwamba M23 imeshindwa, lakini haiwezi kuwa suluhisho tangu 1996 
walipommaliza Mabutu [Sese Seko Kukubanga wa Zabanga], wamekuwa 
wakipigana. Kiongozi wa waasi Laurent Nkunda yuko Uganda (CNDD). Kuna 
nchi ambazo zinatuhumiwa – Rwanda na Uganda zinatuhumiwa,” amesema 
Mugamba. Hata kiongozi wa sasa wa M23, Kanali Sultani Makenga, 
amekimbilia Uganda.
“Sisi
 kama Tanzania tume-play role (tumetimiza wajibu) yetu. Kuna watu 
wanataka haya makundi yawepo kwa sababu wanafanya biashara. Makenga 
alikuwa ana-access dola 58 milioni mwaka jana, tuseme anapata dola 
milioni 10, lazima wote wanafanya biashara.
“Watu
 wote wanaohusika na Congo hebu wakae chini wazungumze. Mali zinauzwa 
nje. Nikiwa Congo niliona vitu ambavyo nasema sawa kuna tatizo, lakini 
mbona kuna mikono mingi tu. Kama hakuna amani Congo au kwa jirani yako, 
wewe huwezi kuwa na amani. Angalia hali ya usalama kwa mikoa ya Kigoma 
na Kagera.
“Jeshi
 la UN lipo Congo kwa miaka 11, watu milioni 5 wameuawa. SADC 
Intervention Brigade UN waliipinga awali, lakini angalia kazi iliyofanya
 kwa miezi sita. Dunia kama ingekuwa na nia ya dhati hawa waasi wote 
wangekuwa hawapo,” anasema Mugamba.
Mobhare
 Matinyi, mchambuzi wa masuala ya kimataifa, anasema M23 kama kikundi 
kimekwisha kwa sababu makamanda wake wamejisalimisha, na kuna taarifa 
kuwa Waziri wa Mashauri ya Nje wa Marekani, John Kerry, na Waziri Mkuu 
wa Uingereza, David Cameron, walimpigia simu Rais wa Rwanda, Paul 
Kagame, kumwambia asiingilie aache hiki kipigo kiishe.
“M23
 imepigika, haina uwezo wa kuibuka tena, lakini bado kuna hatari. Kwa 
kuwa Uganda viongozi wake wana maslahi binafsi nchini Congo na Rwanda 
ina maslahi ya kitaifa Congo, kuna uwezekano wakaanzisha insurgence 
groups (makundi ya waasi) kuleta shida kwa Congo waendelee kuvuna,” 
Matinyi ameiambia JAMHURI.
Anasema
 bado kuna makundi yanayopigana yenyewe kwa wenyewe, baadhi ya makundi 
hayo ni kama FDLR, Democratic Forces for Liberation of Rwanda, mabaki ya
 Interahamwe na Banyamulenge ambao bado ni tishio.
“Majeshi
 yetu Tanzania kihistoria ni nchi yenye msingi wa utu, usawa na haki. 
Ndiyo maana Tanzania imekuwa ikitoa majeshi yake kumtetea Mwafrika na 
kumtetea binadamu. Tulipoitikia kwenda Congo ilikuwa ni kumtetea 
Mwafrika, hatuwezi kukaa miaka 20, 30 watu wakiuawa sisi tunaangalia 
tu,” anasema.
Swali
 ni je, njaa ikiendelea kuwasumbua waasi wa M23 hawatarudi msituni? 
Wachambuzi wanasema mkataba wa amani unapaswa kuharakishwa.
 

 
No comments:
Post a Comment