WAKATI Jeshi la Polisi likiendelea kukwepa kumkamata Mbunge wa Urambo
 Magharibi, Prof. Juma Kapuya (CCM) anayekabiliwa na tuhuma za kumbaka 
mwanafunzi na kutishia kumuua, uongozi wa Bunge umeingilia kati ukitaka 
achukuliwe hatua. 
Chama Cha Mapinduzi (CCM) nacho kimeibuka na kueleza kushangazwa na 
kitendo cha mbunge huyo kuikana namba yake ya simu 0784 993 930 wakati 
ipo hata kwenye kitabu cha wageni cha chama hicho alichokisaini mwenyewe
 mkoani Dodoma.
Prof. Kapuya ambaye amewahi kushika nyadhifa kadhaa za uwaziri katika
 Serikali ya Awamu ya Tatu na Nne, tayari amefunguliwa jalada namba 
OB/RB/21124/13 katika Kituo cha Polisi Oysterbay jijini Dar es Salaam, 
tangu Novemba 24 mwaka huu.
Jalada hilo lilifunguliwa na mwanafunzi huyo anayedaiwa kubakwa na 
kutishiwa kuuawa, lakini Jeshi la Polisi limekuwa likishughulikia suala 
hilo katika namna ya kumlinda mtuhumiwa.
Siku moja baada ya jalada hilo kufunguliwa, Kapuya alidaiwa kutimkia 
nchini Sweden, lakini taarifa za uhakika zinasema kuwa alirejea nchini 
Alhamisi na amekuwa akiishi kwa kujificha huku polisi wakidai kuendelea 
kumsaka.
Ni katika danadana hizo, uongozi wa Bunge umesisitiza kuwa suala hilo ni jinai na linapaswa liende katika mkondo wa kisheria.
Akizungumza na Tanzania Daima wiki hii, Katibu wa Bunge, Dk. Thomas 
Kashililah, alikiri kulifahamu jambo hilo akisema kuwa walipomsikiliza 
mtoto huyo waliona ni suala ambalo linahitaji kushughulikiwa kisheria 
kwa kuwa ni jinai.
“Suala la binti huyo lilifikishwa kwangu kupitia msaidizi wangu 
ambaye alisikiliza hoja na rai yake na kushauriwa kuwa hilo ni suala la 
jinai na linapaswa liende katika mkondo huo.
“Hata hivyo, binti huyo alitambulishwa kwa spika kama kiongozi wa 
wabunge na kuelekeza kuwa tumshauri alifikishe katika mamlaka husika,” 
alisema Dk. Kashililah.
Chanzo chetu cha habari kilithibitisha kuwa binti huyo alikutana na 
Mkuu wa Polisi Wilaya ya Kipolisi ya Oysterbay (OCD) na OC-CID wake na 
kutoa maelezo ya awali kabla ya viongozi hao kumruhusu ayaweke 
malalamiko yake katika maandishi kwa ajili ya kufunguliwa mashtaka.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni, Camilius Wambura, alikiri polisi
 kufungua jalada hilo na kuongeza kwamba hivi sasa wanafanya uchunguzi 
kubaini kama ujumbe ulio katika simu ya binti anayedai kubakwa na 
kutishiwa maisha unatoka katika simu ya mbunge huyo.
Lakini tangu kufunguliwa kwa jalada hilo, mtuhumiwa huyo ameendelea 
kubaki uraiani bila kuhojiwa, huku akiendelea kuwapa vitisho watoto hao,
 kusafiri nje ya nchi na kurejea kupitia Uwanja wa Ndege wa Julius 
Nyerere bila kukamatwa.
Awali Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova
 alipoulizwa kuhusu suala hilo, alisema hawana shamba mjini, kazi yao ni
 kukamata wahalifu na kuwa wangemsaka popote mtuhumiwa huyo ikiwa 
taarifa itafikishwa rasmi polisi.
Kwa siku tatu sasa jeshi hilo limekuwa likitupiana mpira kuhusu kumkamata na kumhoji mtuhumiwa huyo.
Wakati Kamanda Wambura akijitetea kuwa yuko mkoani Arusha, Kamishna 
Kova naye anadaiwa yupo nchini China, huku Kaimu Mkurugenzi wa Makosa ya
 Jinai nchini, Isaya Mungulu akisema hadi jana alikuwa hana taarifa, 
hivyo kuomba muda zaidi ili leo aweze kutolea ufafanuzi.
Uchunguzi wa Tanzania Daima umebaini kuwa Mungulu alikuwa na taarifa 
tangu Kapuya anarejea nchini akitokea nje kwa ndege ya Shirika la Qatar 
ingawa yeye hakuwa tayari kufafanua suala hilo.
CCM wamuumbua
Kada wa Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM) Mkoa wa Dodoma ambaye aliomba 
kuhifadhiwa jina, amemuumbua Prof. Kapuya akisema namba ya simu 
aliyoikana na kudai kuwa alishaigawa miezi sita iliyopita ndiyo hiyo 
aliiandika mwenyewe kwenye kitabu cha wageni.
Akiwa mjini Dodoma kama kamanda wa UVCCM, Kapuya alitembelea tawi 
moja na kusaini kitabu cha wageni ambapo mwisho wa saini yake aliandika 
namba hiyo ya simu ambayo pia imeandikwa kwenye kitabu cha orodha ya 
wabunge.
Kada huyo alisema kuwa alishitushwa kusikia Prof. Kapuya anaikana 
namba 0784 993 930 ambayo imekuwa ikiandikwa na mitandaoni kuwa ndiyo 
imekuwa ikitumika kutuma ujumbe wa vitisho kwa binti anayedaiwa kumbaka.
Alisema kuwa anampa ushauri wa bure Prof. Kapuya asijaribu 
kujiaibisha kwa kuikana namba hiyo kwa sababu hata kwenye moja ya vitabu
 vya wageni aliiandika na kusaini kwa mkono wake.
“25.6.2013 Alhaj Prof. Juma Athuman Kapuya, Mbunge wa Urambo 
Magharibi, Mjumbe wa NEC-CCM Taifa, Kamanda wa UVCCM (M) Tabora, Makamu 
Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu, Juhudi zako 
zibarikiwe na Mungu 0784993930 CCM Oyee,” aliandika Kapuya katika kitabu
 kile.
Source: Tanzania Daima
Source: Tanzania Daima
 

 
No comments:
Post a Comment